Tuesday 9 September 2014

ZITTO KABWE ATOA YA MOYONI NA KUSEMA HAYA KUSUHU WAPAMBE KUMGOMBANISHA NA MBOWE Monday,

Kwa ufupi
Zitto (37), ambaye alikuwa naibu katibu mkuu wa Chadema, alisema kuwa hata kuvuliwa nyadhifa zake ndani ya chama kulisababishwa na wapambe hao, lakini akasisitiza kuwa hana kinyongo tena kwa kuwa alishamwomba Mungu na sasa amesamehe kabisa.

Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ameeleza tofauti yake na mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, akisema imesababishwa na watu aliowaita wapambe.

Zitto (37), ambaye alikuwa naibu katibu mkuu wa Chadema, alisema kuwa hata kuvuliwa nyadhifa zake ndani ya chama kulisababishwa na wapambe hao, lakini akasisitiza kuwa hana kinyongo tena kwa kuwa alishamwomba Mungu na sasa amesamehe kabisa.

Tofauti za wawili hao hazijawahi kutolewa hadharani licha ya mitandao mbalimbali kuzungumzia kuharibika kwa uhusiano wao ikinukuu habari kutoka vikao vya ndani vya Chadema.

Hata hivyo, mapema mwaka huu, Zitto alirushiwa tuhuma nzito na Chadema kutokana na uhusiano wake na baadhi ya makada wa CCM, lakini mbunge huyo aliyahusisha maneno hayo na mwenyekiti wake na aliandika maneno makali dhidi ya Mbowe kwenye ukurasa wake wa facebook.

Lakini katika mahojiano na Mwananchi yaliyofanyika wiki iliyopita nyumbani kwake Masaki jijini Dar es Salaam, Zitto alionekana kujutia kuharibika huko kwa uhusiano wao na kusema “wapambe ndiyo wanatugombanisha”.

“Sina shida yoyote na Mbowe, naamini ipo siku tutagundua wapambe walituathiri na ndiyo waliotufikisha hapa,” alisisitiza Zitto bila kutaja ni kina nani hasa.

Zitto alisema yeye na Mbowe wametoka mbali tangu akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na hafurahii uhusiano wao ukiishia katika hali hiyo.

“Naumia sana, lakini naamini ipo siku ama nikiwa hai au nimekufa watu wataujua ukweli,” alisema mwanasiasa huyo kijana aliyepata umaarufu kutokana na uwezo wake wa kujenga hoja.

Alisema, akiwa mwenyekiti wa Serikali ya wanafunzi wa Chuo Kikuu (Daruso) yeye na mwenyekiti wake ndiyo waliokijenga chama wakati huo Mbowe akiwa mbunge wa Hai.

Alisema wakati huo Mbowe alikuwa akienda chumbani kwake kusuka mikakati ya kuiinua Chadema na kwamba walikuwa wakila chips pamoja na wakati mwingine kwenye klabu ya usiku ya Bilicanas inayomilikiwa na Mbowe.

“Wakati mwingine naangalia, naumia sana. Wakati tunafanya hayo yote wengine walikuwa CCM, wengine walikuwa wafanyabiashara, lakini sasa ndiyo wana sauti katika chama,” alisema Zitto.

Zitto alisema kuwa wakati huo walikuwa na kampeni yao waliyoiita ‘Real Madrid’ ambayo ilikuwa na lengo la kuingiza kila mwanasiasa bora katika chama chao.

Real Madrid ni klabu ya soka ya Hispania yenye mafanikio makubwa duniani na sera yake ni kusajili wachezaji nyota duniani kwa gharama zozote.

“Na kweli tulifanikiwa na kuongeza wabunge kutoka watano hadi 48 wa sasa,” alisema.

“I real miss that (nakumbuka sana). Naumia sana, mimi leo sina maelewano na watu ambao tulikuwa nao katika mapambano. Lakini nasononeshwa zaidi na kitu kinachoendelea ndani ya Chadema.

“Nini kimetokea Chadema? Kwa nini tumejikuta tumeondoka katika mstari? Tupo wabunge 48 bungeni sasa, lakini hatusogezi mbele nchi, tumerudi nyuma wakati huo tulikuwa watano lakini tulikuwa tunaenda vizuri sana.”

Akizungumzia jinsi wapambe walivyoharibu uhusiano wao, Zitto alisema kuna siku Mbowe alimtuhumu kuwa ameanzisha chama cha umma, pia akasema ana majina mawili tofauti katika mtandao wa Jamii forums ambayo anayatumia kuwasema viongozi wa Chadema.

“Kukatokea vurugu, baadaye nikasema naondoka. Ile nataka kutoka wabunge wakanizuia mlangoni nisipite, waliponizuia nilikuwa na hasira sana, nikawaambia lazima nitoke. Waliponizuia hasira zikanipanda nikaanguka chini nikalia sana, yaani sana” alisema akionekana mwenye hisia huku machozi yakimlengalenga.

Kwa mujibu wa Zitto, jioni ya siku hiyo walijikuta wamekaa meza moja na Mbowe na baada ya kuzungumza waligundua kuwa walikuwa wamelishwa maneno.

“Tulizungumza na wote tulilia sana. Wakati kama huu nikikumbuka nasikia uchungu kwa sababu ni wapambe wametufikisha hapa,” alisema.

No comments:

Post a Comment